Alikuwa amenyong’onya huku sura yake ikiwa na makunyanzi. Alinyiririka mithili ya nyoka Nyikani juu ya tanuru lililosheheni mafurushi ya uchafu.
Alikuwa ni kijana mdogo tu kwa kumwangalia huenda alikuwa na umri wa miaka kumi na minne na kwa muda huo alipaswa awe shule akijifunza na wenzie.
Mtima wangu uliingiwa na roho ya huruma, nafsi yangu ikanisukuma miguu nayo ikatii amri. Naam! Nilitembea joshi ili kumuwahi alipokuwa, kutoka katika motokaa yangu aina ya kuruga.
kila nilipomsogelea niliona masagamba yaliyokuwa yameupamba mwili wake mdogo huku ngozi yake ikiwa imepauka kama mtu aliyejipaka unga wa udaga.
Nilisimama kidogo ili kupisha magari yaliyokuwa yanapita, nilivuka barabara kuelekea upande wa lile jalala. Lakini nilipotupa macho sikuweza kumwona tena yule kijana”huenda aliondoka wakati nimesimama ili kuvuka,au wakati naangalia huku na huku kuona kama magari yameisha” niliwaza kisha kwa unyonge nikarudi katika motokaa yangu nikiwa sina amani. Huenda ni kwa vile nilipoteza kitu kilichokuwa mbele ya macho yangu ilihali nilikuwa nakitazamia kwa usawa wa mikono yangu. Moyo wangu uliumia sana kwani Mtoto yule aliniachia maswali mengi kichwani na simanzi kubwa moyoni, nilijiapiza kumtafuta kwa udi na uvumba ili tuu nipate majibu ya maswali ya yangu kwani nilihisi anayamiliki yeye …itaendelea..
